Jinsi ya kupika nyanya chungu na biringanyi za nazi


Muda huu tukutane katika kuandaa mboga inayoenda sana na ugali. Tuna biringanyi, nyanya chungu na bamia, hizi tutaziunga kwa nazi, zitanogaje! Haya tuandae.

Mahitaji

  • Nyanya chungu fungu kubwa 1
  • bamia fungu 1
  • biringanyi kubwa 3
  • pilipili hoho nusu
  • kitunguu  kibwa 1
  • karoti nusu
  • nazi 2
  • nyanya 4
  • mafuta kidogo
  • bizari kiasi (ukipenda)
  • chumvi kiasi
  • pilipili mbuzi 1( kama unatumia)

Jinsi ya kuandaa Hatua kwa hatua

  1. Andaa nyanya, nyanyachungu, bamia na biringanyi zako, kwa kuziosha vizuri kwa maji safi. Kisha  zimenye na kuzikata biringanyi, bamia, nyanyachungu na kuziweka kwenye sahani tayari kwa mapishi.
  2. Andaa hoho, karoti, vitunguu na nazi ikune kabisa, uchuje tui zitozito
  3. bandika sufuria jikoni weka mafuta, yakipata moto  tia vitunguu ukaange, vikibadilika rangi tia hoho endelea kukaanga kidogo kisha tia nyanya ukaange
  4. mimina nyanyachungu na biringanyi na bamia zako na umimine tui la nazi. Tia karoti, chumvi, bizari na usisahau kutupia kapilipili mbuzi ukipenda, koroga uache mchuzi uchemke na nyanyachungu na biringanyi zetu ziive. Zikishaiva mboga yetu itakua tayari.
Naam mboga yetu leo ikipata ugali wakutosha inakuwa safi zaidi. Ila waweza kula na wali ukipenda.