Jinsi ya kupika Makande ya nazi


Jinsi ya kupika Makande: Habari za leo Mpenzi wa blogu hii ya mapishi, natumai u mzima. Karibu tena katika Mapishi ya kitanzania. Leo nakuja na pishi la mlo maarufu, mlo huu ni mchanganyiko wa mahindi na maharage, Makande ya nazi.
Nimekutana na aina nyingi za makande kuanzia shuleni (bweni), safarini na nyumbani, Nimechanganya na vionjo vyangu binafsi kupata makande haya matamu, fuatana nami.

Pishi: Makande ya nazi

Maandalizi

Mahitaji

  • Mahindi yaliyokobolewa Vikombe 2.
  • Maharage Makubwa Kikombe 1.
  • Vitunguu maji vikubwa 2.
  • Nyanya Kubwa 2.
  • Nazi kubwa 1.
  • Pilipili Hoho 2.
  • Binzari kijiko cha chai 1.
  • Mafuta ya kupikia 1/4 kikombe.
  • 9. Chumvi kiasi.
  • 10. Pilipili kali 1.

Utayarishaji na upishi

Namna ya kupika makande hatua kwa hatua

  1. Tayarisha maharage kwa kuyachagua, na kuyaosha vizuri.
  2. Changanya Mahindi na Maharage katika chombo cha kupikia
  3. Weka chumvi kiasi kwenye mchanganyiko huu, kisha pika hadi uive vizuri ila usilainike sana (rojo)
  4. Chemsha mafuta na kaanga vitunguu mpaka viwive na kuwa na rangi ya kahawia.
  5. Ongeza nyanya, karoti, binzari, pilipili hoho, na pilipili kali iliyotwangwa. Kisha Pika mpaka viive.
  6. Changanya vizuri mchanganyiko wa mahindi, maharage pamoja viungo.
  7. Weka chumvi kiasi.
  8. Weka tui la nazi.
  9. Punguza moto na pika kwa dakika tano mpaka kumi.
  10. Makande yako yatakuwa tayari kwa kuliwa.

Jinsi ya kupika makande: Dondoo
Waweza kunyunyizia mchele kidogo wakati mchanganyiko wa mahindi na maharage unaiva ili kuongezea ladha ya makande yako. Pia waweza kutumia maziwa badala ya tui la nazi kama ukipenda.
Hivyo ndivyo namna ya kupika makande ya nazi asante kwa leo.