Vinywaji vya asili


habari wapenzi wa jinsi ya kupika, leo tuzungumzie kuhusu vinywaji vya asili,yaani vinywaji vilivyotokana na mimea na wanyama, mfano miwa, madafu, matunda mbalimbali na maziwa pia.
Inashauriwa kunywa maji kwa wingi si chini ya glasi nane kwa siku ili mwili ufanye kazi vizuri. Vinywaji vya asili huweza kutumika kuongeza kiasi cha maji anachopaswa kutumia mtu. Vinywaji hivi ni pamoja na chai, kahawa, juisi za matunda kama vile maembe, nanasi, machungwa, ukwaju, ubuyu, mabungo na hata maji ya madafu. Vinywaji hivi vinaweza kutengenezwa bila kuongezewa sukari, kwani sukari nayo inamadhara ikitumika kwa wingi.
Vinywaji vya asili vikiandaliwa katika hali ya usafi ni bora na salama kwa afya yako kuliko vinywaji vya viwandani ambavyo huekewa rangi na viongeza ladha visivyoasilia ili kukidhi mauzo kibiashara.

MAMBO YA KUZINGATIA:
  • Pendelea au jenga mazoea ya kutengeneza maji ya matunda nyumbani, hii hupunguza gharama na familia itafaidika kiafya kupata vinywaji asilia
  • Tumia maji yaliyokuwa safi na salama kutengeneza maji ya matunda, hii ni muhimu kwa afya yako na familia, kwani maji yasiosalama huleta magonjwa ya kuhara na homa ya matumbo
  • Punguza matumizi ya sukari nyingi, hakuna haja ya kuongeza sukari kwenye maji ya matunda. Na kwenye chai na kahawa tumia sukari kidogo
  • Kahawa na chai ni vinywaji vyenye viini vinavyozuia ufyonzwaji wa madini ya chuma mwilini. Hivyo inashauriwa kupunguza matumizi yake
Tumia na ujitengenezee nyumbani vinywaji, kwa kutumia matunda kadri yanavyopatikana katika eneo lako. Familia yenye afya bora huwa na furaha. Na mungu akipenda siku zijazo hapa jinsi ya kupika tutaendelea kuelekezana jinsi ya kuandaa vinywaji vya asili aina tofauti tofauti.